Shule ya Upili ya Wasichana ya State House imeripotiwa kufungwa kwa muda usiojulikana kufuatia ghasia za wanafunzi.
Inadaiwa kwamba wanafunzi waligoma kulalamikia hali duni ya maisha, chakula kisichotosheleza, matatizo ya huduma za afya na malalamiko yanayohusiana na masomo.
Hali hii inaongeza wimbi linaloongezeka la ghasia zinazovuruga masomo katika shule za sekondari kote nchini.
Ripoti zinasema wazazi waliombwa Jumatatu kuwachukua wanao baada ya uongozi wa shule kusitisha masomo ili kuruhusu maafisa wa elimu na bodi ya shule kushughulikia malalamiko yaliyotolewa na wanafunzi.
“Tumeekuwa na malalamiko mengi, yakiwemo njaa, huduma za afya, kiwango cha chakula, ubora wa elimu na jinsi wanafunzi wanavyotendewa, huku baadhi wakisema wanachofundishwa hakiendani na viwango vya Wizara ya Elimu,” alisema Mwenyekiti wa Bodi ya shule hiyo.
“Masuala haya yote yatashughulikiwa ili kuhakikisha kuwa wanafunzi watakaporejea, wapate mazingira yanayofaa kwa ajili ya kujifunza.”
Katika taarifa kwa wazazi, uongozi wa shule ulisema hali ya taharuki iliongezeka baada ya baadhi ya wanafunzi kuripotiwa kueleza nia ya kugoma.
Shule ilisema kuwa malalamiko hayo yalisikilizwa na kushughulikiwa, lakini wadau walikubaliana kuwa ilikuwa muhimu kuwaachilia wanafunzi kwa muda ili hali ya utulivu irejee.
“Kulikuwa na kipindi kifupi cha vurugu, kwani baadhi ya wasichana walikuwa wameonyesha nia ya kugoma. Malalamiko yao yalisikilizwa na kushughulikiwa ipasavyo,” taarifa hiyo ilisema.
Kufungwa kwa shule hiyo kunakuja wakati ambapo visa vya ghasia za wanafunzi na matukio yanayoshukiwa kuwa ya uchomaji moto katika shule vinaongezeka katika kaunti kadhaa, hasa maeneo ya Pwani na Kati.