Makala ya 23 ya kipute cha Kombe la Dunia yaliyoanza Juni 11 yanaelekea ukingoni huku mechi 100 zikiwa tayari zimechezwa katika kipindi cha siku 32.
Fainali za mwaka huu ambazo kwa mara ya kwanza zilishuhudia idadi ya timu ikiongezwa kutoka 32 hadi 48 zimekuwa zikifanyika katika viwanja 16 ndani ya miji 16 ya Marekani,Canada na Mexico.
Jumla ya mabao 292 yamefungwa katika michuano 100 ya patashika hiyo,ikiwa wastani wa magoli 2.92 katika kila mechi.
Lionel Messi wa Argentina na Kylian Mbappe wa Ufaransa,wangali wafungaji bora kwa mabao 8 kila mmoja,moja zaidi ya Erling Braut Halaand wa Norway, wakati Harry Kane na Jude Bellingham wa Uingereza, wakiwa wamepachika magoli 6 kila mmoja.
Kila timu iliyobanduliwa katika robo fainali itatuzwa dola milioni 19 sawa na shilingi bilioni 2.4 kila moja,zikiwa Morocco,Uswizi,Norway na Ubelgiji.