Ruto aongoza maadhimisho ya miaka 16 ya Katiba mpya,aelezea hatua zilizopigwa na serikali

Ruto pia alitaja ufanisi mkubwa wa serikali yake katika sekta ya ujenzi na nyumba ambapo nyumba 274,000  za gharama nafuu zimejengwa na kubuni nafasi za ajira zaidi ya milioni 1.1 .

Dismas Otuke
2 Min Read

Rais William Ruto ameongoza maadhimisho ya miaka 16 tangu kurasimishwa kwa katiba mpya ya Kenya mwaka 2010, katika hafla iliyohudhuriwa na viongozi wakuu serikalini katika Ukumbi wa mikutano ya kimataifa (KICC).

Akiongoza sherehe za Katiba Dei ,Ruto ametoa changamoto kwa viongozi wote  kuwa katika mstari wa mbele kuhakikisha utekelezaji kamili wa katiba hiyo ya mwaka 2010, kwa vitendo na wala sio tu nadharia.

Rais alitaja hatua zilizopigwa na utawala wake wa miaka minne, ikiwemo uboreshaji na kuongeza upatikanaji wa huduma za afya kwa wakenya wote,jinsi ilivyoainishwa kwenye katiba kipengee cha 43, ikwa mojawapo wa haki za kimsingi kwa kila Mkenya.

Alifafanua kuwa serikali yake imeafikia maendeleo makubwa katika sekta ya afya ambapo zaidi ya Wakenya milioni 32.4, wamesajiliwa katika bima ya SHA na wengine  zaidi ya milioni 8 wakipokea matibabu katika vituo  mbalimbali vya afya kote nchini.

Aidha, aliongezea kuwa kufikia leo wastawishaji afya ya jamii zaidi ya laki moja wameajiriwa na kutoa huduma kwa familia zipatazo 922 .

Ruto pia alitaja ufanisi mkubwa wa serikali yake katika sekta ya ujenzi na nyumba ambapo nyumba 274,000  za gharama nafuu zimejengwa na kubuni nafasi za ajira zaidi ya milioni 1.1 .

Katika Elimu chini ya Katiba mpya Rais alisema serikali yake imewaajiri walimu zaidi ya laki moja na kujenga madarasa 23,000, hivyo basi kuongeza upatikanaji elimu kwa watoto.

Rais aidha, alisikitishwa na maandamano ya vijana kupinga serikali huku wengine wakiuawa akisema maandamano ni haki ya kila mmoja kulingana na katiba na vijana hao sawa na Mkenya yeyeote walipaswa kulindwa.

Hata hivyo aliwakashifu wavunjanji sheria wanaochukulia fursa ya maandamano ya amani kupora na kuharibu  mali .

Share This Article