Jaji Mkuu Martha Koome ameridhia mradi wa PLEAD II, akisisitiza tena dhamira ya Mahakama ya Kuimarisha mageuzi yanayolenga kuboresha upatikanaji wa haki nchini.
Hii ni baada yake kuongoza kikao cha Kamati Elekezi ya Mradi wa PLEAD II, ambapo Mpango wa Kazi wa Mwaka wa Nne uliidhinishwa.
Kikao hicho kiliwakutanisha wadau mbalimbali muhimu, akiwemo Balozi wa Umoja wa Ulaya nchini Kenya Henriette Geiger na Msajili Mkuu wa Idara ya Mahakama Winfridah Boyani Mokaya.
Wawakilishi wa Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kupambana na Dawa za Kulevya na Uhalifu (UNODC), Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo (UNDP), wanachama wa Baraza la Kitaifa la Utawala wa Haki (NCAJ), mashirika ya kiraia pamoja na washirika wa maendeleo pia walikuwepo.
Kwa mujibu wa Jaji Mkuu Koome, kamati hiyo ilijadili maendeleo yaliyoafikiwa katika kuimarisha sekta ya haki nchini na kuthibitisha tena dhamira ya pamoja ya kutekeleza mageuzi yatakayokuza uadilifu, kuimarisha uwajibikaji, kuharakisha mabadiliko ya kidijitali, kupanua mbinu mbadala za adhabu badala ya kifungo gerezani, na kulinda makundi yaliyo katika mazingira hatarishi.
Alisema hatua inayofuata ya utekelezaji wa mradi wa PLEAD II itajikita katika kuhakikisha mageuzi hayo yanajengeka kikamilifu ndani ya taasisi husika, yanadumishwa kupitia umiliki wa kitaifa, na yanaonekana katika huduma za kila siku kwa Wakenya wanaotafuta haki.
Jaji Mkuu Koome pia aliushukuru Umoja wa Ulaya, Umoja wa Mataifa, taasisi za sekta ya haki pamoja na washirika wengine kwa kuendelea kuunga mkono juhudi za kujenga mfumo wa haki ulio wazi kwa wote, jumuishi, wenye ufanisi na unaoweka mahitaji ya wananchi mbele.