Banky W atangaza kwamba amepona saratani

Marion Bosire
2 Min Read

Mwanamuziki wa Nigeria Olubankole Wellington maarufu kama Banky W ametangaza kwamba sasa yuko huru kutokana na saratani ya ngozi, kufuatia matibabu ya kiwango cha juu.

Banky alichapisha video kwenye akaunti yake ya Instagram iliyomwonyesha akiwa hospitali akiwa na mkewe ambaye ni mwigizaji Adesua Etomi ambaye anaaminika kusimama naye kipindi alikuwa akiugua.

Aliandika, “Ninachapisha ushuhuda huuili kumtia moyo yeyote ambaye anapitia changamoto kama hii. Huenda ukaiona ni kubwa kukuzidi lakini yeye aliye ndani yako ni mkuu kuliko lolote unalopitia haa ulimwenguni.”

Mwimbaji huyo aliendelea kusema kwamba anamshukuru mke wake, familia, marafiki na wahubiri kwa upendo, maombi na usaidizi huku akimshukuru Mungu kwa afya na anaamini kwamba ushindi wake wa hivi punde dhidi ya saratani ndio wa mwisho katika jina la Yesu.

Mwaka 2017, Banky alitangaza kwamba alikuwa amefanyiwa upasuaji kutibu saratani ya ngozi ambayo ilikuwa imegunduliwa yapata miaka kumi kabla ya hapo.

Mashabiki wake kwenye mitandao ya kijamii walifurahishwa na taarifa za ushindi wake dhidi ya saratani huku wakimsifia Adesua kwa kusimama naye muda wote.

Kando na muziki, Banky W wa umri wa miaka 43 hujihusisha na uigizaji, biashara na siasa nchini Nigeria. Alizaliwa nchini Marekani na familia yake ikarejea Nigeria akiwa na umri wa miaka mitano.

Alifunga ndoa kitamaduni na Adesua Etomi Novemba 19, 2017 na harusi ya kanisani ikafanyika nchini Afrika Kusini siku tano baadaye.

Mwaka 2018 na 2023 aliwania ubunge wa eneo la Eti-Osa, katika jimbo la Lagos lakini hakufanikiwa kushinda.

Website |  + posts
Share This Article