Raia nchini Uganda, wameanzisha kampeni mitandaoni ya kuchangisha fedha kwa ajili ya kumuunga mkono mwanasiasa wa upinzani, Dkt. Kizza Besigye, ambaye yuko kizuizini.
Haya yanajiri wakati ambapo wasiwasi unazidi kuongezeka kuhusu hali yake ya afya na muda mrefu aliokaa kizuizini.
Kampeni hiyo, iliyopewa jina la “Stand With Kizza Besigye”, inalenga kukusanya Shilingi milioni 100 za Uganda kwa ajili ya kugharamia mahitaji yake ya matibabu na ustawi, pamoja na kuwasaidia watu wengine waliowekwa kizuizini pamoja naye.
Mwanaharakati wa haki za binadamu, Agather Atuhaire, ambaye ni miongoni mwa waandaaji wa kampeni hiyo, alitangaza Jumapili, Septemba 7, 2026, kwamba michango ilikuwa imefikia Shilingi milioni 22.
“Tafadhali endeleeni kuchangia. Chochote mlicho nacho. Kila mchango wa kuonyesha mshikamano na Kizza Besigye una umuhimu,” Atuhaire aliandika.
Kampeni hiyo imepata michango kutoka kwa wanasiasa, wanaharakati wa haki za binadamu na Waganda wa kawaida, hali inayoonyesha kuendelea kwa wasiwasi kuhusu kuzuiliwa kwa Besigye na ustawi wake.
Miongoni mwa waliochangia ni rais wa chama cha National Unity Platform,NUP, Robert Kyagulanyi Ssentamu, anayejulikana zaidi kwa jina la Bobi Wine na mke wake Barbara Itungo Kyagulanyi, ambao kwa pamoja walichangia Shilingi milioni 5.
Waandaaji wa kampeni hiyo wamewahimiza Waganda zaidi kuchangia ili kufikia lengo la Shilingi milioni 100, wakisema fedha hizo zitasaidia kugharamia mahitaji ya matibabu na ustawi wa Besigye na kuwasaidia wengine waliowekwa kizuizini pamoja naye.
Kampeni hiyo ya uchangishaji fedha inaendelea wakati ambapo hali ya afya ya Besigye na mazingira yanayozunguka kuendelea kuzuiliwa yakiendelea kuvuta hisia za umma.