Kenya imethibitisha tena dhamira yake ya kuimarisha miundombinu ya kidijitali na kupokea teknolojia ibuka ili kuchochea ukuaji wa uchumi na kuiweka nchi katika nafasi ya kuwa kitovu kinachoongoza cha kidijitali barani Afrika.
Katibu wa idara ya Utangazaji na Mawasiliano, Steve Isaboke, alisema hayo katika mkutano wa FiberHome World Tour, Kenya, uliofanyika katika Hoteli ya JW Marriott jijini Nairobi.
Isaboke alisema uwepo wa muda mrefu wa FiberHome nchini Kenya na uwekezaji wake unaoendelea katika mfumo wa kidijitali unachangia kuboresha mawasiliano, kuunda ajira, kuendeleza ujuzi na kukuza ubunifu wa ndani.
Alitaja mipango kama mafunzo maalumu kwa wanafunzi wa Kenya na mpango wa kuanzisha Kituo cha Utafiti na Maendeleo cha Afrika Mashariki, akisema uwekezaji huo unasaidia kujenga uwezo wa ndani katika nyanja zinazoibukia kama akili unde, kompyuta za kisasa, uwekaji wa mifumo kidijitali na mawasiliano ya satelaiti.
Katibu huyo alisema Kenya iko tayari kuendana na mabadiliko katika mitandao ya teknolojia ya habari na mawasiliano kuelekea mawasiliano ya satelaiti, teknolojia salama dhidi ya vitisho na maendeleo kuelekea 6G.
Alisema nchi inaendelea kulenga kupokea ubunifu unaoimarisha miundombinu yake ya kidijitali huku ikiunga mkono ukuaji wa uchumi wa kidijitali.
Isaboke pia alikaribisha uwekezaji na ushirikiano unaolenga kukuza vipaji vya ndani na kuendeleza uwezo wa kiteknolojia.
Alisema mkazo wa Kenya katika ubunifu, maendeleo ya ujuzi na ushirikiano wa kimkakati utasaidia kuiweka nchi katika nafasi ya kuwa kitovu kinachoongoza cha kidijitali barani Afrika.