Wakazi wa wadi ya Gatimu, eneo bunge la Ol joro orok, kaunti ya Nyandarua, wametoa wito kwa halmashauri ya barabara kuu hapa nchini (KeNHA), kujenga njia ya raia wanaotembea kwa miguu kando ya daraja la Riverside katika barabara kuu ya Nyahurury-Olkalou-Gilgil.
Daraja hilo ambalo ndilo mpaka kati ya kaunti ya Nyandarua na Laikipia, hutumiwa na wakazi wa eneo hilo kuelekea Nyahururu mjini, wakiwemo wanafunzi wanaoelekea na kutoka shuleni.
Waliozungumza na shirika la utangazaji nchini KBC, walielezea masikitiko yao kuhusu daraja hilo, wakihoji majukumu ya wabunge kutoka kaunti hizo mbili katika kushughulikia mahitaji ya wakazi, huku watu wakiendelea kuangamia katika daraja hilo.
Wakazi hao sasa wametoa wito wa ukarabati wa daraja hilo kuwajumuisha wanaotembea kwa miguu, ili kuzuia maafa katika eneo hilo.
Daraja la Riverside liko umbali wa kilomita moja unapoingia mji wa Nyahururu kutoka Olkalou,.