Spika wa Bunge la Taifa, Moses Wetang’ula, alikuwa katika eneo bunge la Kitutu Chache Kaskazini kwa mwaliko wa Mbunge wa eneo hilo, Japheth Nyakundi.
Walihudhuria ibada ya Jumapili na baadaye kuongoza mchango katika Kanisa la Orwako PAG lililopo Kitutu Chache North, Kaunti ya Kisii.
“Kanisa ni nguzo kuu ya maadili ya jamii. Tunaendelea kuhimiza Kanisa kuliombea taifa letu ili lidumishe amani na mshikamano,” alisema Wetang’ula.
Alitaja eneo la Gusii kuwa moja ya nguzo muhimu za kilimo nchini Kenya kupitia uzalishaji wa ndizi, kahawa, chai, miwa na mazao mengine.
Spika huyo alisema kwamba chini ya uongozi wa Rais William Ruto, utoaji wa ruzuku unapuuzwa na kuangazia zaidi kuongeza uzalishaji wa kilimo, kuboresha kipato cha wakulima na kuimarisha usalama wa chakula.
“Leo, nilipokuwa nikihutubia wananchi wa Gesieka katika Eneo Bunge la Kitutu Chache Kaskazini, Kaunti ya Kisii, nilithibitisha tena dhamira ya Serikali ya kuendeleza maendeleo endelevu kote nchini” alisema spika huyo.
Pia nilielezea umuhimu wa pendekezo la hazina ya miundombinu na ile ya uwekezaji wa taifa kuwa mageuzi yatakayobadilisha nchi kwa kufadhili uwekezaji muhimu katika barabara, nishati, maji, makazi na miundombinu mingine ya umma, huku yakihakikisha rasilimali za taifa zinawekezwa kwa busara ili kulinda mustakabali wa Kenya.