Kampuni za usafiri kupitia mtandao zapinga udhibiti wa nauli

Kulingana nazo, hatua hiyo huenda ikaongeza gharama za usafiri, kupunguza mahitaji ya abiria na hatimaye kupunguza mapato ya madereva.

Marion Bosire
2 Min Read
John Kiarie, Mwenyekiti Kamati ya Idara ya Mawasiliano, Habari na Ubunifu bungeni

Kampuni za usafiri ambazo huduma zao hupatikana kupitia mtandao, hususan Uber, Bolt na Faras zimeonya Bunge dhidi ya mapendekezo ya kuweka kiwango cha chini cha nauli.

Kulingana nazo, hatua hiyo huenda ikaongeza gharama za usafiri, kupunguza mahitaji ya abiria na hatimaye kupunguza mapato ya madereva.

Wawakilishi wa kampuni hizo walifika mbele ya Kamati ya Idara ya Mawasiliano, Habari na Ubunifu ya Bunge la Kitaifa, inayoongozwa na Mbunge wa Dagoretti Kusini John Kiarie.

Waliwataka wabunge kuendelea kutumia mfumo wa bei unaoamuliwa na soko, kwani mapato ya madereva hayategemei nauli kwa safari pekee, bali pia idadi ya safari, mahitaji ya abiria, matumizi ya magari na gharama za uendeshaji.

Kampuni hizo pia zinapinga kikomo cha sasa cha asilimia 18 cha ada ambazo majukwaa yanaweza kutoza, zikisema kinazuia uwekezaji katika motisha kwa madereva, teknolojia ya usalama, huduma kwa wateja na bidhaa mpya za kidijitali.

Zilipendekeza kikomo hicho kiondolewe huku uwazi na ulinzi wa watumiaji ukiendelea kuzingatiwa.

Aidha, kampuni hizo ziliomba leseni za uendeshaji za miaka mitatu hadi mitano, zikisema uhuishaji wa kila mwaka unasababisha kutokuwa na uhakika.

Wabunge walihoji iwapo madereva hupata mapato ya kutosha baada ya kugharamia mafuta, bima na matengenezo.

Kamati hiyo itazingatia mawasilisho zaidi kabla ya kutoa mapendekezo kuhusu nauli za chini, ada za huduma na mfumo mpana wa udhibiti wa sekta ya usafiri wa mtandaoni nchini Kenya.

Share This Article