China kuadhimisha miaka 80 ya ushindi dhidi ya Wajapani kwa gwaride kubwa Beijing

Viongozi 26 wa kigeni, akiwemo Rais wa Urusi Vladimir Putin na kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong-un, watashiriki maadhimisho ya Siku ya Ushindi nchini China jijini Beijing.

Eric Biegon
4 Min Read

China inajiandaa kwa wakati wa tafakari ya kina na fahari ya kitaifa wakati inaadhimisha kumbukumbu ya miaka 80 tangu ushindi katika vita vya ukombozi wa China dhidi ya Wajapani na vita kuu ya dunia dhidi ya ufaşisti.

Sherehe kuu zitafanyika kesho Septemba 3 katika Uwanja wa Tian’anmen kuanzia saa tatu asubuhi, ambapo Rais Xi Jinping atatoa hotuba kuu na kukagua gwaride la heshima.

Kwa China, kumbukumbu hii si ya kukumbuka historia pekee, bali pia ni ya kuwaheshimu mashujaa waliotoa maisha yao ili kulinusuru taifa. Rais Xi amekuwa akikumbusha raia Wachina mara kwa mara kwamba “taifa lolote lenye matumaini haliwezi kukosa mashujaa”, akisisitiza kuwa moyo wa mapambano – iliyojengwa kupitia mateso na kujitoa mhanga – bado ni chanzo cha nguvu kwa taifa hilo.

Maadhimisho haya, yatakayopeperushwa moja kwa moja na kampuni ya China Media Group na Shirika la Habari la Xinhua, yatakuwa na gwaride la kijeshi lenye vikosi 45 pamoja na ndege za kivita. Kipengele cha kipekee kitapambanua vikosi vya “zamani” vilivyotokana na wapiganaji wa vita vya ukombozi na vikosi vya sasa vinavyoakisi jeshi la kisasa la China. Mpangilio huu unaonyesha daraja kati ya historia na maendeleo ya sasa, na namna China inavyoheshimu urithi wake huku ikisonga mbele kama taifa lililoendelea.

Jioni saa mbili, kutakuwa na tamasha la kumbukumbu katika ukumbi mkuu wa watu, maarufu kama Great Hall of the People, mjini Beijing, ambalo pia litahudhuriwa na Rais Xi. Maelfu ya wanajeshi watapita kwa gwaride, huku silaha na vifaa vya kisasa vilivyotengenezwa nchini vikionyeshwa

Hii ni mara ya pili kwa gwaride maalum la V-Day kufanyika; la kwanza lilifanyika miaka kumi iliyopita. Waandalizi wanasema kuwa mbali na kuonyesha uwezo wa kijeshi wa kulinda mipaka na uhuru, tukio hili pia linalenga kufufua kumbukumbu ya uvamizi wa kigeni, ikiwemo mauaji ya Nanjing ambapo takribani Wachina 300,000 waliuawa.

China inakumbuka kwamba kuanzia 1931 hadi 1945, vita vya ukombozi vilikuwa miongoni mwa vita virefu na vya umwagaji damu zaidi vya vita kuu ya pili ya dunia. Chini ya uongozi wa Chama cha Kikomunisti, CPC, wanajeshi wa China walishiriki maelfu ya mapambano, yakiwemo mapambano ya kikosi mia, na kuisababishia Japani hasara kubwa.

Kwa miongo minne iliyopita, China inasema imejifunza kutokana na historia hiyo ya uchungu, ikipa kipaumbele maendeleo na amani. Rais Xi ameeleza moyo wa mapambano kama kujitolea kwa uzalendo, ujasiri wa kishujaa, na imani thabiti ya ushindi, sifa ambazo amesema ni muhimu kwa Wachina kushinda changamoto na kufanikisha ufufuo mkubwa wa taifa.

Tangu mwaka 2013, China imeweka kumbukumbu rasmi kupitia kuanzisha siku maalum za mashujaa, sheria za kulinda heshima yao na kutoa tuzo za kitaifa. Kwa Beijing, maadhimisho ya kila mwaka ya V-Day ni heshima kwa waliopoteza maisha na pia ni msimamo wa kudhihirisha nafasi yake kama mtetezi wa amani duniani.

Viongozi 26 wa kigeni, akiwemo Rais wa Urusi Vladimir Putin na kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong-un, watashiriki maadhimisho ya Siku ya Ushindi nchini China jijini Beijing.

Share This Article