Huduma ya Taifa ya Polisi, NPS imetangaza kukamatwa kwa washukiwa 15 wanaodaiwa kupanga kuvuruga shughuli za kisiasa, katika msako kwenye barabara ya kutoka Kisumu kuelekea Kericho.
Katika taarifa ya leo Agosti 16, 2026, NPS ilisema washukiwa hao walikamatwa jana katika oparesheni iliyotokana na taarifa za kijasusi, huku polisi wakidai kuwapata wakiwa na silaha mbalimbali.
Washukiwa hao kwa sasa wako chini ya ulinzi wa polisi na wanatarajiwa kufikishwa mahakamani huku uchunguzi ukiendelea.
Matokeo ya awali ya uchunguzi yanaonyesha kuwa watu hao walidaiwa kuajiriwa kazi ya kusababisha vurugu wakati wa shughuli za kisiasa katika eneo hilo.
Polisi wamewaonya wanasiasa, waandaaji wa hafla na wananchi dhidi ya uchochezi, ushawishi wa vurugu na mwenendo wowote unaoweza kuhatarisha amani na usalama.
NPS pia imeelekeza maafisa wanaotumwa kwenye hafla za kisiasa na mikusanyiko ya umma kuzingatia weledi, kutokuwa na upendeleo na kujizuia, huku wakilinda haki ya wananchi kufanya mikusanyiko ya amani.
Wananchi wanahimizwa kuripoti shughuli za uhalifu au zinazotiliwa shaka katika kituo cha polisi kilicho karibu au kupitia njia zilizowekwa, zikiwemo nambari za dharura 999 na 911, #FichuakwaDCI na nambari yake ya WhatsApp.
Huduma ya Kitaifa ya Polisi imesisitiza kuwa haina upendeleo wa kisiasa na imejitolea kulinda haki za kikatiba, utulivu wa umma na utawala wa sheria.