Mwimbaji wa nyimbo za injili nchini Kenya Denno amefurahisha mashabiki zake katika mitandao ya kijamii kupitia simulizi ya kuchekesha na yenye mafunzo kuhusu ziara yake jijini Mombasa.
“Iwapo unaniuliza nilichoona Mombasa, jibu langu huenda likakukatisha tamaa kidogo kwa sababu sikuona pembe maarufu za ndovu za Mombasa,” alianza ujumbe wake kwenye Facebook huko akiweka ishara za kicheko.
Denno ambaye hana uwezo wa kuona, alitania kuwa wakati watalii wengine walikuwa wakipiga picha kwenye pembe maarufu za ndovu jijini Mombasa, yeye alikuwa akijitahidi kuhakikisha hagongi moja yazo kwa bahati mbaya.
Msanii huyo alisema kuwa kutokuwa na uwezo wa kuona kumemfundisha kufurahia uzuri wa sehemu mbalimbali kwa njia tofauti na wale walio na uwezo wa kuona.
Alitoa mfano wa Mombasa ambayo anasema alifurahia kupitia upepo mwanana wa bahari, sauti za jiji, harufu ya chumvi ya bahari na ukarimu wa watu aliokutana nao.
Pia alijibu kwa ucheshi waliouliza kwa nini hakuwa anaangalia pembe hizo za ndovu wakati wa kupigwa picha, akisema alimwamini mpiga picha wake, akiongeza kuwa, “Wakati mwingine, imani hukupeleka mbali zaidi kuliko macho.”
Chapisho hilo limepokelewa vyema na watumiaji wengi wa mitandao ya kijamii, ambao wamemsifu Denno kwa kuunganisha ucheshi, shukrani na ujumbe wa kutia moyo unaokumbusha kwamba uzuri halisi wa maisha mara nyingi huhisiwa moyoni kuliko kuonekana kwa macho.