Viongozi kutoka ukanda wa Pwani wametakiwa kuwa mstari wa mbele katika kupiga jeki maswala ya elimu katika ukanda huo.
Kwa mujibu wa Mawaziri Salim Mvurya wa Madini na Uchumi wa Baharini na Aisha Jumwa wa Jinsia, Utamaduni na Turathi za Kitaifa, ukanda huo umeendelea kusalia nyuma katika masuala ya elimu.
Wakizungumza katika mji wa Malindi, kwenye hafla ya maombi na ufunguzi wa shule ya Town Secondary, mawaziri hao wamesema kuwa elimu ndiyo nguzo kuu ya maendeleo ya jamii katika kaunti ya Kilifi na pwani kwa jumla, kwani inahakikisha kizazi cha baadaye kinapata maisha bora.
Ukosefu wa walimu wa kutosha katika shule kadhaa umekuwa chanzo cha matokeo duni huku viongozi hao wakielezea kusikitishwa na hatua ya idadi kubwa ya wanafunzi katika shule za upili katika kaunti ya Kilifi kupata matokeo duni.