Marekani na Kanada zimeafikia makubaliano ya kuzuia ushuru mkubwa kwa bidhaa za Kanada zenye thamani ya mabilioni ya dola, Rais wa Marekani Donald Trump ametangaza.
Trump alitoa tangazo hilo muda mfupi kabla ya kuisha kwa muda wa mwisho wa saa sita usiku wa kuweka ushuru wa asilimia 50 kwa bidhaa mbalimbali zinazouzwa na Kanada nchini Marekani, kama vifaa vya kielektroniki, mashine za viwandani, samani na bidhaa za maziwa.
“Nimesitisha ushuru wa asilimia 50 dhidi ya Kanada, ambao ulipangwa kuanza kesho asubuhi kwa kipindi cha siku tatu, kutokana na ukweli kwamba Kanada na Marekani, zikisubiri kukamilishwa kwa nyaraka, WAMEFIKIA MAKUBALIANO!” Trump aliandika katika chapisho kwenye Truth Social.
“Bomba kubwa la Keystone XL, ambalo zamani liliuawa na ‘Sleepy Joe’ Biden, huenda likaamshwa kutoka kaburini!” aliongeza kiongozi huyo wa Marekani.
Kulingana naye, makubaliano yakikamilika huenda yakaruhusu kufufuliwa kwa mradi wa bomba hilo la mafuta la Keystone XL, ambalo lingeunganisha Mkoa wa Alberta wa Canada na Marekani na ambalo anadai lilizuiwa na tawala za Obama na Biden.
Canada na Marekani zimekuwa katika mkwamo kuhusu masuala kadhaa, ikiwa ni pamoja na ushuru wa Marekani kwa magari na majimbo mengi ya Kanada kupiga marufuku uuzaji wa pombe kutoka Marekani.
Trump na Waziri Mkuu wa Canada Mark Carney walizungumza mara mbili wiki hii, huku wawakilishi wa biashara wakiwa katika mazungumzo makali tangu Julai, baada ya Trump kutishia kuweka ushuru huo mpya na kuweka tarehe ya mwisho kuwa Agosti 19.