Madonna aahirisha ziara baada ya kuugua

Marion Bosire
1 Min Read

Mwanamuziki mkongwe wa Amerika Madonna Louise Ciccone, maarufu kwa jina lake moja Madonna, ameahirisha ziara yake wiki chache kabla ya tarehe iliyokuwa imewekwa baada ya kulazwa hospitalini. Mwimbaji huyo wa umri wa miaka 64 amelazwa katika chumba cha wagonjwa mahututi kufuatia maambukizi ya maradhi yanayotokana na bakteria.

Meneja wa Madonna, Guy Oseary, alitangaza hayo jana Jumatano kupitia Instagram akielezea kwamba alianza kuugua Jumamosi, Juni 24 na akalazwa hospitalini lakini hali yake inaendelea kuboreka wakitarajia atapona kabisa.

Oseary alielezea kwamba wamelazimika kusitisha kwa muda mipango yote ya Madonna ikiwemo ziara.

Aliahidi kutangaza tarehe mpya za ziara hiyo pamoja na tarehe za matamasha mengine ambayo pia yameahirishwa.

Ziara hiyo ambayo ilikuwa imepatiwa jina la “The Celebration tour” ya kuadhimisha miaka 40 ya Madonna katika tasnia ya burudani ilikuwa imepangiwa kuanza Julai 15, 2023 huko Vancouver, Canada.

Madonna alipanga ziara hiyo kutokana na mchezo wa “Truth or Dare” mwezi Januari ambapo mchekeshaji Amy Schumer alimchochea afanye ziara ya ulimwengu na aburudishe watu kwa muziki wake.

Mashabiki wa gwiji huyo wa muziki aina ya pop, hata hivyo, watalazimika kusubiri kwa muda kabla ya kumwona na kumsikiliza huku wakimwombea dua apone.

Website |  + posts
Share This Article