Kenya yatwaa ubingwa wa Riadha Afrika

Kikosi cha Kenya kilichowajumuisha wanariadha 74 kilinyakua dhahabu 6 fedha 4 na shaba saba.

Dismas Otuke
2 Min Read

Kenya iliibuka mabingwa wa Afrika katika makala ya 24 yaliyokamilika jana Jumapili jijini Accra, Ghana kwa jumla ya nishani 17.

Kikosi cha Kenya kilichowajumuisha wanariadha 74, kilinyakua dhahabu 6, fedha 4, na shaba saba.

Julius Yego alinyakua dhahabu na kuhifadhi taji lake la urushaji sagai la mwaka 2024, likiwa taji la sita la mashindano hayo.

Washindi wengine wa dhahabu walikuwa Diana Chepkemoi katika mita 3,000 kuruka viunzi na maji, Edwin Too aliyeshinda dhahabu ya kwanza ya Kenya ya Decathlon, Kelvin Loti Kimtai katika mita 800, Kevin Chesang na Diana Wanza katika mita 10,000.

Fedha nne za Kenya zilinyakuliwa na Silvia Jerono na Stephen Ndagiri katika shindano la matembezi kilomita 20, Mercy Chepngeno katika mita 3,000 kuruka viunzi na maji, na  timu ya mita 400 kwa wanariadha wanne kupokezana kijiti wanaume.

Kenya ilishinda nishani za shaba katika urukaji wa kimo kupitia kwa Asbel Kiprop na Belinda Oburu katika urushaji tufe.

Washindi wengine wa shaba za Kenya walikuwa Laban Kiptoo katika mita 5,000, Silas Senchura mita 10,000, Isaac Ndute katika urukaji mapana na timu ya wanawake ya mita 400 kwa wanawake kupokezana kijiti, na mita 400 kwa wanariadha wanne kupokezana kijiti jinsia mchanyato.

Ilikuwa mara ya kwanza kwa Kenya kunyakua taji la jumla tangu mwaka 2022 mjini Porto Novo, Benin.

Afrika Kusini ilimaliza ya pili kwa  nishani 14, sita dhahabu, fedha 2 na shaba 2, huku Ethiopia, ikifunga tatu bora kwa dhahabu 5, fedha 4 na shaba 6.

Share This Article