Kenya na China leo Alhamisi, zimetia saini mikataba 20 ya biashara na maelewano ya kuimarisha sekta mbali mbali za uchumi wa Kenya.
Rais William Ruto na mwenzake wa China Xi Jinping, waliongoza hafla ya kutiwa saini kwa mikataba hiyo katika ukumbi wa Great Hall of the People mjini Beijing, China.
Kupitia ukurasa wake wa X, kiongozi wa taifa alisema ushirikiano kati ya Kenya na China ni wa kudumu na unaowanufaisha wananchi wa nchi hizo mbili.
Kulingana na kiongozi wa taifa, washirika wa China watapata fursa ya kuwekeza raslimali zao katika uimarishaji wa barabara za humu nchini , Elimu, Kilimo,Uchumi wa majini, Kawi safi na Teknolojia ya Habari na Mawasiliano.
“Mikataba hii ni thihirisho kuwa China inaunga mkono juhudi zetu za kukuza uchumi wetu, kubuni nafasi za ajira kwa vijana wetu pamoja na kustawisha rasilimali za taifa hili,” alisema Rais Ruto.
Kuhusu diplomasia rais Ruto alisema walikubalina ana rais Xi kuendelea kuimarisha umoja na ushirikiano na eneo la kusini mwa dunia.
Viongozi hao wawili pia walikubaliana kuendelea kuthibiti na kufanyia marekebisho sera za umoja wa mataifa hasa katika baraza la usalama la umoja huo ili uweze kutekeleza majukumu yake ipasavyo.