Katibu katika Wizara ya Afya Mary Muthoni amelalamikia matumizi ya mihadarati miongoni mwa vijana hasa watoto wa shule.
Amehusisha tabia hiyo na nyakati zinazobadilika na upatikanaji wa mihadarati hiyo kwa urahisi.
Kulingana naye, matumizi ya mihadarati sasa yanafikia viwango hatari kwani inapatikana kwa urahisi mno hata nje ya shule.
Katibu Muthoni aliyasema hayo jana Alhamisi jioni alipowaandalia waumini wa dini ya Kiislamu chakula cha jioni cha Iftar.
Alionya dhidi ya kuwatambulisha watoto kwa mihadarati kama vile bangi na sigara akisema kuna wafanyabiashara wasiojali maslahi ya watoto hao kamwe kando na kupata faida.
Sasa anawataka viongozi wa kidini kuwa mstari wa mbele kuwaelekeza vijana katika mienendo inayofaa katika jamii.