Crazy Kennar kuanzisha onyesho mubashara

Marion Bosire
1 Min Read
Crazy Kennar

Kennedy Odhiambo maarufu kama Crazy Kennar ambaye ni mwigizaji na mchekeshaji wa mitandaoni ana mpango wa kuanzisha onyesho la moja kwa moja au ukipenda mubashara.

Kupitia video aliyochapisha kwenye mitandao, Kennar alisema anataka kuanzisha kitu ambacho hata yeye kinamtia woga na shauku lakini anaamini ndoto hiyo inawezekana.

Alisema onyesho hilo anapanga kulianzisha mwezi Disemba mwaka huu na aliomba wafuasi wake wamsaidie kusambaza matangazo ya onyesho hilo wakati ukiwadia na wanunue tikiti kwa wingi na kuhudhuria.

Mwanzo wa video hiyo mchekeshaji huyo anasikika akisema kwamba alipoanza uigizaji mitandaoni, hakudhania kwamba utamfungulia milango mingi na kwamba angepata umaarufu alioafikia.

“Nakumbuka mzazi mmoja aliniambia kwamba mwanawe alikuwa akiniiga na kwamba mimi ni baraka kwa kizazi cha sasa. Huwa ninabeba maneno ya mzazi huo kila siku.” alisema Kennar.

Crazy Kennar ameshangaza wengi kwa kuendelea na kazi yake na kufanikiwa hata zaidi baada ya kutengana na washirika wake wa awali.

Kwa sasa ana washirika wapya kwenye video zake za mitandaoni. Alianza kuandaa na kuchapisha kazi za mitandaoni mwaka 2017 na sasa anataka kuwapiku waandalizi wa maonyesho ya vichekesho nchini kwa kuandaa onyesho litakalohudhuriwa na watu elfu 6 kwa wakati mmoja.

Jina la onyesho lake huenda likawa “Happy Country”.

https://www.instagram.com/reel/CxZ5CtFtqE9/?utm_source=ig_web_copy_link&igshid=MzRlODBiNWFlZA==

Website |  + posts
Share This Article