Rais William Ruto ameanza ziara yake kukagua na kuzindua miradi ya maendeleo katika kaunti ya Kajiado mapema leo Alhamisi, huku akiwahimiza wakazi kuepuka siasa za uchochoezi na propaganda.
Ruto alianza ziara hiyo kwa kukagua barabara ya umbali wa kilomita 67 ya Illasit-Rombo-Chala-Njukini-Taveta eneo la Oloirien,kaunti ya Kajiado.
Barabara hiyo inayogharimu shilingi bilioni 9.4, itarahisisha uchukuzi punde itakapokamilika na kufungua fursa za kiuchumi kupitia usafirishaji wa mizigo na watu huku muda wa kusafiri kutoka Kajiado hadi Taveta, ukitarajiwa kupungua hadi saa mbili na dakika 40 pekee .
Barabara hiyo iliyoanza kujengwa Juni mwaka jana imefikia asilimia 48 na inatarajiwa kukamilika mwezi Machi mwaka ujao.
Pia barabara hiyo itaunganisha mbuga za wanyama za Amboseli na Tsavo na kurahisisha biashara kati ya Kenya na Tanzania.