Ndejembi apendekezwa kuwa Makamu wa Rais Tanzania

Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM iliidhinisha kwa kauli moja uteuzi wa Ndejembi .

Marion Bosire
1 Min Read

Chama tawala nchini Tanzania CCM, kimemteua Waziri wa Nishati, Deogratius John Ndejembi, kuchukua wadhifa wa Makamu wa Rais wa Tanzania, kufuatia kujiuzulu kwa Emmanuel Nchimbi.

Nchimbi alitangaza Agosti 25 kuwa atajiuzulu nafasi ya Makamu wa Rais na kustaafu siasa pamoja na utumishi wa umma, huku uamuzi huo ukianza kutekelezwa Septemba 4, 2026.

Rais Samia Suluhu Hassan alikubali kujiuzulu kwake.

Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM iliidhinisha kwa kauli moja uteuzi wa Ndejembi baada ya uongozi wa chama kuzingatia jina lake, katika kikao kilichofanyika jana.

Ndejembi, ambaye amewahi kuwa Waziri wa Nishati na ni Mbunge wa Chamwino, anatarajiwa kushika moja ya nyadhifa za juu zaidi za kisiasa nchini Tanzania iwapo mchakato wa kikatiba utakamilika.

Kwa mujibu wa Katiba ya Tanzania, wadhifa wa Makamu wa Rais unapokuwa wazi, Rais huteua mrithi ambaye uteuzi wake lazima uthibitishwe na Bunge kwa kura za wengi.

Katiba pia inataka uteuzi huo ufanyike ndani ya siku 14 baada ya nafasi hiyo kuwa wazi.

Hivyo, Ndejembi atalazimika kupata ridhaa ya Bunge kabla ya kuanza rasmi majukumu ya Makamu wa Rais.

Share This Article