Wizara ya Afya yazindua utoaji chanjo dhidi ya Polio Kaskazini Mashariki

Tom Mathinji
2 Min Read
Mary Muthoni - Katibu katika Wizara ya Afya

Wizara ya Afya imezindua kampeni ya utoaji chanjo dhidi ya ugonjwa wa kupooza wa Polio, kuanzia Februari 21 hadi 25, katika kaunti za  Marsabit, Wajir, Garissa na Mandera.

Kupitia kwa taarifa iliyotolewa leo Ijumaa, katibu katika wizara ya Afya Mary Muthoni, alisema kampeni hiyo inawalenga watoto  176,949  walio chini ya umri wa miaka 11 Marsabit na watoto  651,252 walio chini ya umri wa miaka tano  katika kaunti za Wajir, Garissa na Mandera.

Awamu nyingine ya utoaji chanjo imepangwa kutekelezwa mwezi Aprili katika kaunti hizo hizo, ambazo zimetambuliwa kukabiliwa na hatari kubwa ya maambukizi kutokana na idadi ndogo ya wanaopewa chanjo na shughuli za mpakani.

Katibu Muthoni alisema hatua ya kampeni hiyo inajiri baada ya ugonjwa wa Polio kuthibitishwa kuzuka nchini Ethiopia katika eneo la Moyale Oktoba mwaka 2024, kilomita 15 kutoka mpaka wa Kenya.

“Ni muhimu kudokeza kuwa katika kila kisa kilichothibitishwa, kuna zaidi ya visa 200 ambavyo havijathibitishwa na hivyo ipo haja ya kuchukua hatua kuzuia maambukizi,” alisema katibu Muthoni.

Alitoa wito kwa wazazi na walezi kuhakikisha watoto wao wanachanjwa hata ikiwa walichanjwa hapo awali, ili kuzuia kuenea kwa ugonjwa huo.

“Tunahakikishia umma kwamba chanjo inayotolewa ni salama  na imefanyiwa uchunguzi wa kina. Kupokea chanjo mara zaidi ya moja hakuna madhara kwa mtoto wako, lakini kunaongeza kinga dhidi ya magonjwa,” aliongeza katibu huyo.

Alitoa wito kwa wananchi kuripoti visa vyovyote vinavyoshukiwa kuwa vya Polio katika kituo cha afya kilicho karibu au kupitia nambari za simu za wizara ya Afya 719, 0729 471414, au 0732 353535.

Share This Article
Leave a Comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *