Rais Ruto aapa kuhakikisha utawala wa sheria unadumishwa

Martin Mwanje
1 Min Read

Rais William Ruto amewaonya waratibu wa maandamano yanayoendelea kuwa serikali itakabiliana vikali na wale wanaodhamiria kukiuka utawala wa sheria. 

Ruto amesema wahalifu ni lazima wakabiliwe vikali.

“Wakati wa kampeni, tuliahidi kuwa tutakomesha hulka ya kuvunja sheria bila kuadhibiwa. Kama tu tulivyoahidi kwamba polisi hawatahusika katika mauaji ya watu kiholela, ndivyo ambavyo tumejitolea kuhakikisha hakuna atakayevunja sheria bila kuadhibiwa,” alisema Rais Ruto alipozungumza katika shule ya upili ya Mugoiri, kaunti ya Murang’a leo Ijumaa.

Alisema serikali yake itahakikisha kila mtu anaheshimu utawala wa sheria akiongeza kuwa uvunjaji wa sheria bila kuadhibiwa  hautakubalika kwa namna yoyote.

“Hauwezi ukavunja sheria bila kujali na kusababisha vurugu bila kuwajibishwa,” alionya Rais.

Aliwapongeza maafisa wa usalama kwa namna walivyoshughulikia maandamano ya siku tatu ya Azimio yanayomalizika leo Ijumaa.

Muungano wa Azimio uliitisha maandamano hayo kwa lengo la kuishinikiza serikali kupunguza gharama ya juu ya maisha.

Watu kadhaa wameripotiwa kufariki wakati wa maandamano hayo na wengine kujeruhiwa.

Website |  + posts
Share This Article