Wetangula ataka usambazaji sawa wa walimu

Spika huyo anasema kwamba licha ya serikali kuajiri walimu wengi na kupanga kuongeza wengine, shule za vijijini bado zina upungufu.

Marion Bosire
2 Min Read

Spika wa bunge la taifa Moses Wetangula ameibua wasiwasi kuhusu upungufu wa walimu katika shule za maeneo ya vijijini, akitoa wito kwa Wizara ya Elimu kuchukua hatua za haraka kushughulikia pengo hilo.

Akizungumza katika Shule ya Sekondari ya Wasichana ya St. Francis Kolongolo katika Eneo Bunge la Kwanza, Spika huyo alielezea hali hiyo kuwa ya dharura na isiyokubalika.

Wetangula alibainisha kuwa licha ya serikali kuajiri zaidi ya walimu 100,000 na kupanga kuongeza wengine 20,000, baadhi ya taasisi za vijijini bado zinakabiliwa na upungufu mkubwa wa walimu.

Alieleza kuwa Shule ya Sekondari ya Kolongolo pekee ina upungufu wa hadi walimu 28, hali ambayo alisema inadhoofisha ubora wa elimu kwa wanafunzi wa maeneo yaliyotengwa.

Huku akitambua juhudi za Rais William Ruto katika kuboresha uwiano wa walimu kwa wanafunzi kitaifa, Wetangula alisisitiza kuwa maendeleo hayo yanapaswa kusikika kote nchini.

Alisisitiza kuwa upangaji wa walimu unapaswa kuzingatia usawa na mahitaji halisi, badala ya upendeleo wa vituo vya mijini.

Spika huyo pia alielekeza wito wake kwa Waziri wa Elimu Julius Ogamba, akitaka mageuzi katika sera za upangaji wa walimu ili kuhakikisha usambazaji sawa.

Aidha, Wetangula alihimiza viongozi wa eneo hilo kuepuka siasa za mgawanyiko na badala yake kuhimiza umoja, akisisitiza kuwa eneo hilo linaakisi utofauti mkubwa wa Kenya na linapaswa kubaki mfano wa mshikamano na ushirikiano.

Share This Article