Kampuni za Pepsi na Diageo zimeondoa udhamini wao kwa tamasha la Wireless nchini Uingereza ambapo Kanye West amealikwa kutumbuiza baada ya Waziri Mkuu Keir Starmer kulikosoa.
Rapa huyo wa Marekani amekuwa akikosolewa kutokana na matamshi yake ya chuki dhidi ya Wayahudi.
Mwanamuziki huyo wa umri wa miaka 48 alitumbuiza mwisho mwaka 2015 na anatarajiwa kuwa msanii mkuu kwa siku zote tatu za tamasha hilo katika eneo la Finsbury Park jijini London mwezi Julai.
Msemaji wa Pepsi alisema, “Pepsi imeamua kujiondoa katika ufadhili wa Tamasha la Wireless.”
Kampuni ya Diageo, ambayo inamiliki vinywaji vya Johnnie Walker na Captain Morgan, pia ilisema Jumapili jioni kuwa imejiondoa.
Msemaji alisema waandaaji tayari wamearifiwa kuhusu wasiwasi wa kampuni hiyo akiongeza kwamba Diageo haitafadhili tamasha la Wireless la mwaka 2026.
West alijipata pabaya kufuatia machapisho ya chuki dhidi ya Wayahudi kwenye mtandao wa X, tangazo la Super Bowl lililoelekeza watu kwenye fulana yenye alama ya swastika na wimbo unaomsifia Hitler.
Sir Keir alisema ni jambo la kutia wasiwasi mkubwa kwamba West amealikwa licha ya matamshi yake ya awali ya chuki dhidi ya Wayahudi na kusifu Unazi.
“Chuki ya aina yoyote dhidi ya Wayahudi ni mbaya na lazima ipingwe wazi na kwa uthabiti popote inapojitokeza. Kila mtu ana jukumu la kuhakikisha Uingereza ni mahali ambapo Wayahudi wanajihisi salama na kulindwa,” alisema waziri mkuu.
Mwezi Januari, West aliweka tangazo la ukurasa mzima kwenye gazeti la Wall Street akiomba msamaha. Tangazo hilo lilikuwa na mada; “Kwa Wale Niliowaumiza.”
aliendelea kujieleza akisema yeye sio Mnazi wala sipingi Wayahudi na kwamba anapenda Wayahudi.
West alihusisha matamshi yake ya awali na ugonjwa wake wa bipolar-1, ambao anasema umemsibu kwa muda mrefu na humfanya kutekeleza vitendo anapokuwa na msisimko na kujutia baadaye.
Hapo awali, West alipoteza mkataba wake na Adidas kufuatia chapisho lake la mwaka 2022 kwenye mitandao ya kijamii, ambapo aliweka picha ya alama ya swastika ndani ya Nyota ya Daudi.
Muda mfupi baadaye, alikosolewa kwa tangazo la televisheni lililowaelekeza watu kwenye tovuti iliyokuwa ikiuza fulana zenye picha ya swastika na akatoa wimbo ulioitwa “Heil Hitler”.
Sir Ed Davey, kiongozi wa wanachama huria wa chama Democratic, wiki iliyopita alitoa wito kwa serikali kumpiga marufuku West kuingia Uingereza.
Alisema Waziri wa Mambo ya Ndani Shabana Mahmood anapaswa “kumpiga marufuku kuja nchini — tunapaswa kuchukua chuki dhidi ya Wayahudi kwa uzito zaidi.”