Marekani yamuokoa rubani aliyepotea baada ya ndege kuangushwa Iran

KBC Digital News
2 Min Read

Mwanajeshi wa Marekani ambaye alikuwa amepotea tangu Iran ilipoangusha ndege ya kivita ameokolewa, kulingana na ujumbe wa Rais Donald Trump aliouandika kwenye mitandao ya kijamii mapema Jumapili.

Operesheni kubwa ya utafutaji na uokoaji ilianzishwa mara moja baada ya ajali ya ndege ya F-15E Strike Eagle iliyotokea Ijumaa, huku Iran pia ikiahidi zawadi kwa yeyote ambaye angemkabidhi rubani huyo. Mwanakikosi wa pili aliokolewa mapema kabla ya hapo.

Katika ujumbe wake, Trump alimuelezea rubani huyo kama shujaa aliyekuwa amenaswa ndani ya eneo hatari milimani nchini Iran, akifuatiliwa kwa karibu na maadui. Alisema licha ya kujeruhiwa, hali yake si mbaya na anatarajiwa kupona, akibainisha kuwa operesheni ya uokoaji ilihusisha ndege nyingi na ufuatiliaji wa saa zote kabla ya kufanikisha zoezi hilo.

Ndege hiyo ya kivita ndiyo ya kwanza ya Marekani kuanguka ndani ya ardhi ya Iran tangu kuanza kwa mzozo huo mwishoni mwa Februari. Tukio hilo limeonyesha hatari inayokabili wanajeshi wa Marekani katika operesheni zao, hasa katika mazingira yenye ulinzi mkali wa adui.

Wiki iliyopita, Trump alidai kuwa Marekani ilikuwa imeidhoofisha vibaya Iran na ingeumaliza mzozo huo haraka. Hata hivyo, siku chache baadaye Iran iliangusha ndege mbili za kijeshi za Marekani, jambo lililoonesha kuwa licha ya kushambuliwa, bado ina uwezo wa kujibu mashambulizi na kuendeleza mapambano.

Share This Article