DRC yapokea watu 15 waliorejeshwa kutoka Marekani

KBC Digital News
2 Min Read

Watu 15 waliorejeshwa kutoka Marekani wamewasili katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).

Waliofukuzwa waliwasili katika mji mkuu, Kinshasa, usiku wa kuamkia Ijumaa ikiwa ni sehemu ya makubaliano kati ya Marekani na DRC.

Chanzo cha kidiplomasia kililiambia wanahabari kuwa kundi la kwanza, linalojumuisha wanawake saba, linaundwa na raia wa Peru na Ecuador.

Afisa mmoja wa idara ya uhamiaji ya DRC alithibitisha kuwasili kwao lakini hakutoa maelezo zaidi.

Wakili wa Marekani, Alma David, anayemwakilisha mmoja wa waliorejeshwa, alisema wote wanatoka Amerika ya Kusini, na kwamba serikali ya DRC inapanga kuwahifadhi nchini humo kwa muda mfupi.

Kwa mujibu wake, wahusika hao wote walikuwa na ulinzi wa kisheria kutoka kwa majaji wa Marekani uliowazuia kurejeshwa katika nchi zao za asili.

Mapema mwezi huu, Wizara ya Mawasiliano ya DRC ilitangaza kuwa itakubali kwa muda wahamiaji wanaorejeshwa kutoka Marekani, huku Washington ikitarajiwa kugharamia gharama zote zinazohusika na maandalizi ya makazi karibu na Kinshasa.

Shirika la habari la Reuters liliripoti kuwa DRC ilitarajiwa kupokea zaidi ya watu 30 wiki hii, huku wengine wakitarajiwa kuwasili kwa makundi ya takriban watu 50 kila mwezi, ingawa idadi ya jumla bado haijafahamika.

Shirika la Kimataifa la Uhamiaji (IOM) limesema kuwa DRC iliomba msaada wa kibinadamu kutoka Umoja wa Mataifa ili kuwahudumia wahamiaji hao.

Share This Article