Bill Cosby apatikana na hatia katika kesi nyingine ya ubakaji

Anadaiwa kumnyanyasa kingono Donna Motsinger, baada ya kumpa divai na vidonge mwaka 1972.

Marion Bosire
2 Min Read

Jopo la waamuzi wa kiraia huko California lilipata Jumatatu kwamba Bill Cosby ana hatia ya kumpa dawa na kumdhulumu kingono mwanamke mwaka 1972 na kumtaka amlipe fidia ya dola milioni 19.25.

Baada ya kesi iliyodumu karibu wiki mbili huko Santa Monica, wajumbe wa jopo la waamuzi walimpata Cosby wa umri wa miaka 88 na hatia ya unyanyasaji wa kingono dhidi ya Donna Motsinger.

Wakili wa Cosby, Jennifer Bonjean, alisema kupitia barua pepe kwamba wamesikitishwa na wanakusudia kukata rufaa dhidi ya uamuzi huo.

Uamuzi huo ulitolewa karibu miaka mitano baada ya Cosby kuachiwa huru kutoka gerezani huko Pennsylvania, baada ya Mahakama Kuu ya jimbo hilo kufuta hukumu ya jinai iliyotokana na madai sawia.

Motsinger alikuwa mhudumu katika mkahawa huko Sausalito karibu na San Francisco, na alisema katika kesi yake iliyowasilishwa mwaka 2023 kwamba Cosby alimwalika kwenye onyesho lake la vichekesho katika ukumbi wa michezo ulioko San Carlos.

Wote wawili walikuwa katika miaka yao ya thelathini wakati huo.

Alisema Cosby alimpa divai na vidonge viwili alivyodhani ni aspirini na kwamba alikuwa anapoteza fahamu na kurejea katika hali ya fahamu huku wanaume wawili wakimweka kwenye gari la kifahari.

Mahakama ilifahamishwa kwamba Donna Motsinger aliamka nyumbani kwake bila nguo zote isipokuwa nguo za ndani na alijua alikuwa amepewa dawa na kubakwa na Bill Cosby.

Katika nyaraka za mahakamani, mawakili wa Cosby walidai kwamba madai hayo yanategemea kwa kiasi kikubwa dhana na makisio, wakisema Motsinger anakiri wazi kwamba hajui kilichotokea.

Jopo la waamuzi lilimpa Motsinger dola milioni 17.5 kwa madhara ya awali na dola milioni 1.75 kwa madhara ya baadaye.

Share This Article