Wanamuziki nyota wa Afrika Mashariki Bien na Joshua Baraka wamepangiwa kutumbuiza jijini Kigali nchini Rwanda, katika kipindi cha mapumziko kwenye mashindano ya Ligi ya Afrika ya Mpira wa Kikapu, BAL.
Bien atatumbuiza Mei, 22, 2026 kwenye usiku wa ufunguzi wa hatua ya mwondoano kwenye ukumbi wa BK Arena, huku Joshua Baraka akitarajiwa kupanda jukwaani Mei 23, 2026 kama sehemu ya tamasha la mapumziko ya kipindi cha ligi lijulikanalo kama “Live at the BAL”.
Wasanii hao wawili wamewahi kushirikiana mara kadhaa, hivi karibuni zaidi wakishirikiana katika wimbo “Ayayaah,” wa mtayarishaji na mwimbaji wa Rwanda Element Eleéeh.
Bien pia alionekana kwenye remix ya wimbo uliompa umaarufu mkubwa Nana wa Joshua Baraka pamoja na King Promise na Joeboy, ushirikiano uliosaidia kupanua mashabiki wa Baraka kote ukanda huu.
Akitambulika sana kama mwanachama wa kundi la muziki wa afro-pop la Kenya Sauti Sol, Bien ameendelea kujenga mafanikio katika kazi yake binafsi kwa maonyesho mbalimbali barani Afrika na kwingineko.
Joshua Baraka pia amejiimarisha kama mmoja wa wasanii chipukizi wanaong’ara Afrika Mashariki, akijulikana kwa kuchanganya aina mbalimbali za muziki huku akitayarisha na kupiga ala za muziki.
Anarejea Kigali miezi michache tu baada ya kutumbuiza katika tamasha ya Tempah’s Reset 2026 iliyofanyika katika kituo cha Mundi mapema mwaka huu.
Hatua ya mwondoano ya BAL 2026 itashirikisha timu nane, RSSB Tigers, Petro de Luanda, Al Ahly Ly, Dar City, ASC Ville de Dakar, Club Africain, FUS Rabat na Al Ahly. Fainali imepangwa kufanyika Mei 31 katika BK Arena.
Ratiba ya burudani itahitimishwa usiku wa fainali kwa burudani kutoka kwa mwimbaji wa Tanzania Abigail Chams.
Msimu wa BAL 2026 ulianza Machi 27 kwa Kongamano la Kalahari mjini Pretoria, South Africa, na utahitimishwa kwa fainali jijini Kigali.