Rais aliyeondolewa mamlakani nchini Niger Mohamed Bazoum ameiomba jumuiya ya kimataifa ichukue hatua za haraka kuirejesha serikali yake mamlakani.
Anasema iwapo mapinduzi yaliyotekelezwa na wanajeshi yatafanikiwa, yatakuwa na athari mbaya kwa ulimwengu mzima.
Taarifa ya kiongozi huyo ilichapishwa na jarida la Washington Post, ambapo aliomba Marekani na nchi nyingine zisaidie nchi yake kurejelea utawala wa kikatiba.
Bazoum, anachukulia nchi ya Niger kuwa ambayo ndiyo ya kuleta matumaini katika eneo zima la Afrika magharibi, ambapo nchi kadhaa zimeathirika na uvamizi wa makundi ya kigaidi na mapinduzi.
Alielezea kwamba Niger ndiyo nchi pekee ambayo inaheshimu haki za kibinadamu katika eneo la Sahel wakati ambapo nchi nyingine jirani zimeingiliwa na mashirika ya kiimla.
Anahisi kwamba eneo la Sahel huenda likatawaliwa na kundi la Wagner kutoka Urusi ambalo ukatili wake umeonekana bayana nchini Ukraine.
Niger, ilikuwa koloni ya Ufaransa na ilijipatia uhuru mwaka 1960.
Nchi hiyo inayopakana na Libya, Chad na Nigeria, imekuwa ikipokea usaidizi wa kiwango cha juu wa kijeshi kutoka kwa Marekani. Usaidizi huo unakisiwa kuwa wa thamani ya dola milioni 500 tangu mwaka 2012.