Maafisa wa tume ya maadili na vita dhidi ya ufisadi hapa nchini (EACC), wamemkamata afisa wa polisi kwa madai ya kuchukua hongo kaunti ya Nyandarua.
Luke Nyasangah, ambaye ni afisa wa upelelezi wa maswala ya jinai DCI katika kituo cha polisi cha Ngano, kaunti ya Nyandarua, alikamatwa baada ya kumuitisha mkazi wa eneo hilo shilingi 10,000 ambaye alikuwa ameibiwa shilingi 115,000.
Mkazi huyo alikuwa anatafuta usaidizi wa afisa huyo wa polisi, ili amsaidie kupata fedha hizo zilizoibwa.
Kulingana na tume hiyo ya EACC, afisa huyo wa polisi alimwambia mkazi huyo kuwa fedha hizo ni za lazima, ili msako dhidi ya wezi hao uanzishwe.
Mshukiwa huyo sasa anazuiliwa katika kituo cha polisi cha Charagita, akisubiri kufikishwa mahakamani.