Afisa wa Kikosi cha Iran auawa katika shambulizi – vyombo vya habari

radiotaifa
2 Min Read
Picha kwa hisani ya AFP

Taarifa ya BBC:

Msemaji na afisa wa uhusiano wa umma wa Kikosi cha Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (IRGC) ameuawa katika mashambulizi ya Marekani na Israel, vyombo vya habari vya Iran vinaripoti.

Ali Mohammad Naini alihudumu katika kikosi cha IRGC kwa miongo minne, akihudumu kama msemaji wa shirika hilo kwa miaka miwili iliyopita, linaripoti shirika la habari la Fars linaloshirikiana na IRGC.

Milipuko mikubwa zaidi yaripotiwa Tehran

Israel imekuwa ikishambulia mji mkuu wa Iran, Tehran, kwa mashambulizi ya anga huku Wairani wakisherehekea Nowruz – Mwaka Mpya wa Uajemi.

Usiku kucha, Iran pia ilirusha makombora kuelekea Yerusalemu. Milio mikubwa ya uzuiaji ilisikika mara kwa mara juu ya ardhi usiku kucha.

Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu hapo awali aliwaambia waandishi wa habari kwamba Iran sasa “imesambaratishwa” na haiwezi kurutubisha madini ya urani au kutengeneza makombora ya balistiki.

Wiki hii, Iran ilipolipiza kisasi kwa shambulio la Israel kwenye kiwanda chake kikubwa cha gesi cha South Pars, bei za mafuta duniani zilipanda. Sasa zimeanza kushuka kutokana na ahadi ya Israeli ya kujiepusha na mashambulizi kama hayo na mipango ya Marekani ya kuongeza uzalishaji wa mafuta.

Pia kulikuwa na taarifa ya pamoja Alhamisi jioni, ambapo Uingereza, Ufaransa, Japani na wengine walielezea kile walichosema ni “utayari wao wa kuchangia juhudi stahiki ili kuhakikisha usalama” katika Mlango-Bahari wa Hormuz.

Share This Article