Abba Marcus kufikishwa mahakamani Marekani wiki ijayo

Anakabiliwa na shtaka moja la shambulio la nyumbani.

Marion Bosire
2 Min Read

Abba Marcus Mayanja wa miaka 20, mwanawe mwanamuziki nguli wa Uganda Jose Chameleone, anatarajiwa kufikishwa mahakamani Minnesota, nchini Marekani Jumatatu, Agosti 17, 2026.

Hii ni baada yake kukamatwa kwa tuhuma za shambulio la nyumbani, kosa ambalo ni la kiwango cha chini, kwa mujibu wa kumbukumbu za mahabusu za Kaunti ya Hennepin.

Abba anatarajiwa kufikishwa katika mahakama ya Ridgedale saa tatu unusu asubuhi, baada ya polisi wa Edina kumkamata Agosti 14 na kumweka rumande saa 1:18 mchana.

Anakabiliwa na shtaka moja la shambulio la nyumbani linalodaiwa kuhusisha kitendo kilicholenga kumfanya mtu ahofie madhara ya haraka ya mwili au kifo.

Iwapo atapatikana na hatia, anaweza kuhukumiwa kifungo cha hadi siku 90 jela, faini ya hadi dola 1,000 za Marekani, au vyote viwili. Adhabu hiyo ya juu kabisa haimaanishi kwamba atahukumiwa moja kwa moja kifungo cha jela.

Adhabu yoyote itategemea matokeo ya kesi na tathmini ya mahakama.

Katika kusikilizwa kwake kwa mara ya kwanza, mahakama inatarajiwa kumweleza rasmi shtaka linalomkabili na haki zake za kisheria, ikiwemo kupata wakili na iwapo atastahili, wakili wa serikali.

Jaji pia anaweza kuamua kuhusu dhamana na masharti ya kuachiliwa, masharti ambayo yanaweza kujumuisha amri ya kutowasiliana na mlalamikaji, vikwazo vya kusafiri au hatua nyingine.

Familia ya Mayanja haijatoa maoni hadharani kuhusu kukamatwa kwake. Kukamatwa huko kulitokea baada ya uhusiano wake na mpenzi wake mjamzito kuvurugika hadharani.

Share This Article