Ruto: Tutabuni mjadala wa kitaifa kuhusu mustakabali wa nchi

Rais Ruto alidokeza kuwa mjadala huo haulengi kubuni mpango mpya wa serikali, lakini hatua hiyo inahusu kuwa na makubaliano ya pamoja na viwango vya ubora vya kukadiria hatua zinazopigwa.

Tom Mathinji
1 Min Read
William Ruto - Rais wa Kenya.

Rais William Ruto, amesema serikali itabuni mjadala wa kitaifa kuhusu mustakabali wa taifa hili baada ya kukamilika kwa ruwaza ya mwaka 2030.

Kwenye hotuba yake kwa taifa Alhamisi usiku, kiongozi wa taifa alidokeza kuwa uzinduzi huo utakaotekelezwa Agosti 12, 2026,  utampa kila Mkenya fursa ya kushiriki kwenye mjadala huo kupitia utoaji maoni kwa mara ya kwanza tangu kubuniwa kwa katiba ya taifa hili ya mwaka 2010.

“Tunapaswa kujiuliza ni yapi tunapaswa kutekeleza tofauti kuhakikisha ukurasa mpya wa maendeleo ya taifa hili ni tofauti na ule wa awali,” alisema Rais Ruto.

Aidha, Rais Ruto alidokeza kuwa mjadala huo haulengi kubuni mpango mpya wa serikali, lakini hatua hiyo inahusu kuwa na makubaliano ya pamoja na viwango vya ubora vya kukadiria hatua zinazopigwa.

Kulingana na Ruto, ruwaza itakayoongoza Kenya katika kizazi kijacho, lazima ibuniwe kupitia mchakato unaowajumuisha wananchi na unaozingatia siku zijazo.

“Ruwaza itakayotoa mwelekeo wa Kenya katika kizazi kijacho, haiwezi kutayarishwa na serikali. Haiwezi kubuniwa na wataalam wachache pekee, taasisi fulani au wanasiasa,” alisema Rais Ruto.

Share This Article