Rais William Ruto amewasili Jijini Evian, Ufaransa kwa mkutano wa viongozi wa G7, ambako anawakilisha bara Afrika mbele ya chumi kuu zaidi duniani.
Kiongozi huyo wa taifa ameandamana na Mama Taifa Rachel Ruto na Mkuu wa Mawaziri aliyepia Waziri wa Mambo ya Nje Musalia Mudavadi.
Ruto anahudhuria mkutano huo kwa mwaliko wa Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron, ambaye ndiye mwenyeji wa Kongamano hilo akiwa Rais wa sasa wa kundi la G7, ambalo linashirikisha mataifa saba ambayo chumi zao zimeimarika zaidi duniani.
Kwenye mkutano huo, Ruto anajiunga na viongozi wengine wa dunia kujadili maswala muhimu yanayohusu dunia, ikiwa ni pamoja na biashara ya kimataifa, kukabiliana na tabianchi, usalama, uchumi na akili unde.
Miongoni mwa viongozi watakaohudhuria mkutano huo ni pamoja na Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron, Donald Trump (Marekani), Waziri Mkuu wa Canada Mark Carney, Chansela wa Ujerumani Friedrich Merz, Waziri Mkuu wa Italia Giorgia Meloni, Waziri Mkuu wa Japan Sanae Takaichi na Waziri Mkuu wa Uingereza Keir Starmer.