Wahusika wa maandalizi ya filamu iitwayo “A Blue Butterfly” wako nchini Rwanda kwa ajili ya kunakili sehemu za filamu hiyo.
Kulingana na mswada wa filamu hiyo, maeneo ya maandalizi ya filamu hiyo ni London na Rwanda.
Maandalizi ya kazi hiyo ya sanaa yanaripotiwa kuwa katika hatua za mwisho mwisho na matukio yaliyosalia ni ya nchini Rwanda pekee.
C.J. “Fiery” Obasi wa asili ya Nigeria ndiye mwelekezi wa filamu hiyo waigizaji wakuu wakiwa Steve Toussaint na Sanaa Lathan. Wengine ni Lucian Msamati, Anton Lesser na Eliane Umuhire wa asili ya Rwanda.
A Blue Butterfly ni simulizi kuhusu mwanaume mmoja ambaye anaishi katika upweke kihisia ambaye anakwazwa sana na hisia za hatia.
Akiwa anafanya kazi kama dereva wa gari la kifahari, mwanaume huyo anaendelea kuwa mbali na dunia hadi anapokutana na mwigizaji wa kike, na kuanza kubadili mtazamo wake.
Filamu hii inachunguza mada za kiwewe, uhai na kutafuta ukombozi, ikijitokeza kupitia mwingiliano wa karibu wa wahusika badala ya matukio makubwa ya kuvutia macho.
Mradi huu pia unaashiria kurejea kwa Obasi katika utengenezaji wa filamu za urefu kamili kufuatia filamu yake iliyosifiwa Mami Wata ya mwaka 2023 iliyoonyeshwa katika tamasha kubwa za kimataifa.
Filamu hii ilichaguliwa kuwakilisha Nigeria kwa kipengele cha Filamu Bora ya Kimataifa katika Tuzo za 96 za Akademia na kupata uteuzi katika tuzo za Independent Spirit na NAACP Image.