Tamasha ya utamaduni wa Lamu kupiga jeki utalii

Tom Mathinji
1 Min Read

Maandalizi ya kila mwaka ya sherehe za kitamaduni za Lamu awamu ya 21, yamepamba moto, huku wageni 3,000 wakitarajiwa kuhudhuria.

Katika sherehe hizo, utamaduni wa wakazi wa Lamu huonyeshwa, na kwa miaka kadhaa, sherehe hizo zimewavutia watalii wa humu nchini na wale wa kimataifa.

Gavana wa kaunti ya Lamu Issa Timammy amesema sherehe hizo zitaandaliwa kuanzia Novemba 30 hadi Disemba 2 mwaka huu.

Kulingana na Gavana huyo, tamasha ya mwaka huu itakuwa na maonyesho ya ziada ikiwemo soka ya ufuoni, kwa kuwa vijana watatu wako katika timu ya taifa ya kandanda ya ufuoni.

Mashindano mengine yatakayoshuhudiwa katika tamasha hiyo ni pamoja na voliboli, mashindano ya mbio za punda na uogeleaji.

“Nawakaribisha Wakenya wote na pia raia wa kigeni kuungana nasi wakati wa tamasha hiyo ya utamaduni wa Lamu itakayodumu kwa siku tatu,” alisema Gavana huyo.

Aliongeza kuwa tangu makala ya mwaka jana ya tamasha hiyo, shughuli za kitalii zimeongezeka katika kaunti ya Lamu.

Kwa upande wake, Waziri wa Utalii na Biashara wa kaunti ya Lamu Aisha Miraj alisema wanatafuta wafadhili kuhakikisha tamasha hiyo inafaulu.

“Kwa sasa  Lamu ni salama. Watu wanasafiri kwa miguu na pia ndege zinawaleta watalii,” alisema Miraj.

Website |  + posts
Share This Article