Serikali itatumia kitita cha shilingi bilioni 25 kwa ujenzi wa barabara mpya katika kaunti ya Embu.
Naibu Rais Prof. Kithure kindiki amesema fedha hizo zitatumika kujenga kilomita 412 za barabara mpya katika kaunti hiyo, hatua ambayo itafanikisha uchukuzi wa bidhaa na watu na pia kuunganisha eneo hilo na sehemu zingine za nchi.
“Serikali inaharakisha uwekaji lami wa barabara ya kilomita 19.2 ya Kanyuambora-Kamumu- Soko Mjinga- Kageeri- Siakago kwa shilingi bilioni 2.7,” alisema Prof. Kindiki.
Aliyasema hayo alipokuwa akikagua ujenzi wa daraja la Ena, eneo ambalo limeshuhudia ajali nyingi za barabarani na kusababisha maafa hasa nyakati za msimu wa mvua.

Awali, alikagua ujenzi wa soko la kisasa la Karurumo katika kaunti ya Embu ambalo ujenzi wake utagharimu shilingi milioni 60.