Serikali imebuni majukwaa ya kuwawezesha wanafunzi na vijana kuonyesha talanta zao kwa njia huru, ujasiri na ubinifu. Hayo yamesemwa Ijumaa na Rais wa Kenya William Ruto.
Kiongozi wa taifa alidokeza kuwa sanaa ina nafasi muhimu katika nchi hii, kwa kuwa huelezea utamaduni, turathi na maisha ya kila siku yanayohusu maswala mbali mbali.
Akizungumza wakati wa tamasha maalum iliyoandaliwa katika Ikulu ya Nairobi baada ya kukamilika kwa makala ya 64 ya kitaifa ya michezo ya kuigiza na filamu, Rais Ruto alisema tamasha za michezo ya kuigiza na filamu miongoni mwa shule mbalimbali nchini ni muhimu kwa ustawi wa wanafunzi na zinapaswa kuungwa mkono kama kiungo muhimu cha elimu.
Rais aliongeza kuwa sanaa za ubunifu, ikiwa ni pamoja na tamthilia, muziki na filamu, zina jukumu muhimu katika kukuza ujuzi na vipaji miongoni mwa vijana.
Aidha, aliagiza kufadhiliwa kikamilifu kwa michezo hiyo ya kuigiza na filamu na wizara ya elimu na kuifanya kuwa njia mwafaka na rasmi za masomo nchini.
Tamasha hiyo maalum ilikuwa kilele cha burudani ya siku kumi na mbili iliyoandaliwa kuanzia tarehe 6 hadi 17 mwezi huu katika Kaunti ya Nyeri.