Rais William Ruto amesisitiza tena dhamira ya serikali yake ya kuwezesha vijana kupitia uwekezaji katika sekta ya michezo na maeneo mengine muhimu yanayolenga kuunda ajira na kupanua fursa nchini kote.
Akizungumza katika Ikulu ya Nairobi jana, Rais Ruto alisema serikali inawekeza katika michezo, uchumi wa ubunifu na kidijitali, ajira za nje ya nchi, makazi ya gharama nafuu, msaada kwa biashara na maendeleo ya miundombinu ili kuwawezesha vijana kuchangia mageuzi ya taifa.
Rais alibainisha kuwa serikali inajenga na kuboresha viwanja 34 vya michezo kote nchini ili kuendeleza vipaji na kuboresha mazingira ya wanamichezo wanaochipukia.
Alisema uwekezaji huo tayari unaanza kuzaa matunda, akitaja mafanikio ya wanariadha wa Kenya katika mashindano ya kimataifa pamoja na kufuzu kwa kihistoria kwa timu ya Junior Harambee Starlets kushiriki Kombe la Dunia la FIFA la Wanawake walio chini ya umri wa miaka 17.
Kiongozi wa nchi Rais William Ruto aliikaribisha Migori Youth FC, mabingwa wa Ligi ya Taifa ya Super msimu wa 2025/2026 na kuikabidhi rasmi basi jipya litakalorahisisha usafiri wa timu hiyo katika mechi zake za ligi kote nchini.
Rais pia alitangaza kuwa serikali inajenga uwanja wa kisasa wa michezo katika Kaunti ya Migori ili kuipatia timu hiyo na jamii kwa ujumla mazingira bora ya kukuza vipaji vya wenyeji, akieleza kuwa michezo ni nguzo muhimu ya kuwawezesha vijana na kuchochea ukuaji wa uchumi nchini Kenya.