Maafisa wa polisi Afrika Kusini wanaendelea na uchunguzi kuhusu misururu ya mauaji ya wananwake, huku mwili wa tisa ukipatikana katika eneo la Ekurhuleni Jijini Johannesburg.
Kulingana na polisi, miili mitatu kati ya minane ambayo ilipatikana awali, ilikuwa katika eneo hilo ikiwa nusu uchi wiki hii.
Mwili wa muathiriwa wa hivi punde ulipatikana ukiwa nusu uchi na ukiwa umefungwa kwenye shuka kando ya barabara, polisi wakisema bado haujatambuliwa.
Msururu huo wa mauaji ya wanawake umeibua wasiwasi kwa umma, kitendawili kikiwa iwapo yanatekelezwa na muuaji mmoja.
“Uchunguzi unaangazia uwezekano iwapo washukiwa kadhaa wanahusika,” alisema Kamishna wa polisi wa mkoa wa Gauteng Fred Kekana.
Rais Cyril Ramaphosa siku ya Jumatano, alisema juhudi zitafanywa kuwapata waliohusika na vifo hivyo ambavyo vimeibua hofu nchini humo.