Marekani na Iran zakosa kuafikia makubaliano ya amani

Mazungumzo ya amani yaliandaliwa jijini Islamabad nchini Pakistan.

Marion Bosire
2 Min Read
JD Vance na Shehbaz Sharif jijini Islamabad

Marekani na Iran zimeshindwa kuafikia makubaliano ya amani baada ya mazungumzo ya hali ya juu yaliyofanyika katika mji mkuu wa Pakistan.

Makamu wa Rais JD Vance alisema kwamba Tehran ilikataa kukubali masharti ya Washington baada ya saa 21 za mazungumzo mjini Islamabad.

“Habari mbaya ni kwamba hatujafikia makubaliano, na nadhani hiyo ni habari mbaya zaidi kwa Iran kuliko ilivyo kwa Marekani,” alisema Makamu wa Rais JD Vance, kiongozi wa ujumbe wa Marekani.

Alikuwa akizungumza na waandishi wa habari muda mfupi kabla ya kuondoka Islamabad baada ya mkutano wa ngazi ya juu zaidi kati ya Washington na Tehran tangu mapinduzi ya Kiislamu ya mwaka 1979.

Vance alisema Iran ilichagua kutokubali masharti ya Marekani akiongeza kuwa Marekani inahitaji kuona dhamira ya msingi ya kutotengeneza silaha za nyuklia kutoka Tehran.

Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran ilisema Jumapili kwamba hakuna aliyetarajia mazungumzo na Marekani kuafikia makubaliano katika kikao kimoja.

Msemaji wa wizara hiyo Esmaeil Baghaei alisema kwamba Tehran ilikuwa na imani kwamba mawasiliano kati yake na Pakistan, pamoja na marafiki wao wengine katika eneo hilo yataendelea.

Wakati huo huo, Pakistan ilizitaka Marekani na Iran kuheshimu ahadi yao ya kusitisha mapigano na kuendelea na juhudi za kufikia amani ya kudumu.

Marekani na Israel zilianzisha vita dhidi ya Iran tarehe 28 Februari, vita vilivyoenea katika Mashariki ya Kati, huku Tehran ikifanya mashambulizi ya kulipiza kisasi dhidi ya Israel na nchi jirani za Ghuba zinazohifadhi rasilimali za Marekani.

Zaidi ya watu 2,000 wameuawa na maeneo ya kijeshi na kiraia kuharibiwa katika mashambulizi ya Marekani na Israel dhidi ya Iran.

Vita hivyo pia vilisababisha mgogoro wa nishati duniani baada ya Iran kuweka vizuizi katika Mlango wa Hormuz ambako takriban asilimia 20 ya mauzo ya mafuta na gesi duniani hupitia.

Share This Article