Rais William Ruto amesema kampuni tatu kubwa za muziki duniani zimekubali kuanzisha shughuli zao jijini Nairobi, hatua aliyoieleza kuwa mafanikio makubwa kwa sekta ya ubunifu nchini Kenya.
Katika taarifa aliyochapisha baada ya kukutana na Victoria Oakley, Afisa Mkuu Mtendaji wa Shirikisho la Kimataifa la Sekta ya Rekodi za Muziki, IFPI, Ruto alisema Sony Music, Universal Music Group na Warner Music Group zimeonyesha dhamira ya kupanua shughuli zao katika soko la Kenya.
Rais alisema uamuzi huo unaonyesha kuongezeka kwa imani ya kimataifa katika vipaji vya ubunifu vya Wakenya, sera za serikali na mageuzi yanayoendelea yenye lengo la kujenga sekta ya muziki inayoweza kushindana kimataifa.
Ruto alibainisha kuwa mazungumzo hayo yalihusu kuimarisha uchumi wa ubunifu wa Kenya na kuiweka Nairobi kuwa kitovu kikuu kijacho cha sekta ya muziki uliorekodiwa barani Afrika.
Alisema hatua inayofuata itakuwa kutekeleza mikakati itakayounda mazingira bora kwa wasanii, watayarishaji wa muziki, wachapishaji wa kazi za muziki na wawekezaji kustawi kwa pamoja.
Kwa mujibu wa Rais, uwekezaji huo unatarajiwa kufungua fursa mpya kwa wabunifu wa Kenya, huku ukichochea ajira na kuongeza mauzo ya muziki wa Kenya katika masoko ya kimataifa.
Ruto alisisitiza kuwa mageuzi yanayotekelezwa na serikali yanalenga kuhamasisha ubunifu na kuvutia kampuni kubwa za kimataifa kuwekeza katika sekta ya ubunifu inayokua kwa kasi nchini.