Rais Ruto ampongeza Wanyonyi kwa rekodi mpya

Alivunja rekodi ya mita 1000 ya miaka 27, iliyowekwa na Noah Ngeny.

Marion Bosire
2 Min Read

Rais William Ruto amempongeza mwanariadha wa Kenya Emmanuel Wanyonyi kwa kuvunja rekodi katika Monaco Diamond League.

Kiongozi wa nchi alichapisha picha ya mwanariadha huyo iliyo na muda wake mpya wa mbio za mita elfu 1 na kuandika, “Pongezi kwa Emmanuel Wanyonyi kwa kuvunja rekodi ya dunia ya mbio za mita 1000 kwa wanaume kwa muda wa kipekee wa dakika 2:11.83 katika Mashindano ya Diamond League ya Monaco, na hivyo kumaliza miaka 27 ya rekodi iliyokuwepo ya dunia katika mbio hizo.”

Ruto anasema mafanikio haya ya kihistoria ya Wanyonyi yameonyesha tena ulimwengu ubora na nguvu ya riadha ya Kenya, na yamelifanya taifa hili kujivunia kwa kiwango kikubwa.

“Hatua hii ya kipekee itahamasisha vizazi vingi vijavyo vya mabingwa kufuata nyayo zake” alimalizia Rais.

Emmanuel Wanyonyi alianza mbio zake za kwanza kabisa za mita 1000 kwa mtindo wa kuvutia, akitumia dakika 2:11.83 kuvunja rekodi ya dunia iliyodumu kwa muda mrefu katika mashindano hayo ya Monaco jana Ijumaa Julai 10, 2026.

Bingwa huyo wa Olimpiki na dunia wa mbio za mita 800 alipunguza sekunde 0.13 kutoka rekodi ya dunia ya 2:11.96 iliyowekwa na Mkenya mwenzake Noah Ngeny huko Rieti mwaka 1999.

Wanyonyi alifuata wakimbiaji wa kuongoza mwendo, huku wa kwanza, Patryk Sieradzki, akifikisha mita 400 kwa muda wa sekunde 50.95, uliolingana na kasi ya kuvunja rekodi ya dunia kama ilivyopangwa.

Share This Article