Taarifa ya Bruno Mtunga
Kampeni za kiti cha ubunge cha Isiolo Kusini zimefikia hatua ya mwisho huku uchaguzi mdogo ukitarajiwa kufanyika Alhamisi wiki hii. Viongozi wa kisiasa katika kaunti hiyo, akiwemo Gavana Abdi Guyo na mbunge wa kaunti Mumina Bonaya, wameanzisha kampeni kali za mlango kwa mlango na koo kwa koo wakimuunga mkono mgombea wa UDA, Tubi Mohamed Tubi, katika wadi za Kinna na Sericho mtawalia.
Uchaguzi huo umechukua sura ya ushindani wa kindugu, ukimkutanisha Tubi Mohamed Tubi wa chama cha UDA dhidi ya dada yake Bina Tubi anayewania kiti hicho kupitia tiketi ya chama cha Jubilee. Kiti hicho kilibaki wazi kufuatia kifo cha baba yao, Mohamed Tubi Bidu, mwezi Novemba mwaka jana.
Mgombea mwingine, aliyekuwa Mwakilishi Wadi (MCA) wa Wadi ya Kinna, Isaack Abduba Fayo, ambaye alikuwa ameidhinishwa na Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) kuwania kupitia chama cha National Economic Development Party (NEDP) kilichosajiliwa na aliyekuwa Gavana wa Nairobi Mike Mbuvi Sonko, alijiondoa katika kinyang’anyiro hicho siku tatu zilizopita baada ya kukutana na Rais W illiam Ruto.
Fayo sasa anaunga mkono mgombea wa UDA.
Huku uchaguzi ukitarajiwa kufanyika Alhamisi, Februari 26, Gavana Guyo jana Jumapili alikita kambi katika Wadi ya Kinna huku Mumina akifanya kampeni eneo la Modogashe katika Wadi ya Sericho, wakifanya mikutano kadhaa na wanachama wa koo mbalimbali kwa nyakati tofauti. Viongozi hao wawili wanamtetea na kumpigia debe mgombea wa UDA.
Akizungumza katika eneo la Kulamawe, Wadi ya Kinna, Gavana Guyo aliwahimiza wakazi kujitokeza kwa wingi kupiga kura na kutekeleza haki yao ya kikatiba ya kumchagua kiongozi wao. Aliwataka kumuunga mkono mgombea wa chama tawala cha UDA, akisema kuwa eneo hilo litanufaika zaidi kwa kuwa sehemu ya serikali badala ya kuwa upinzani.
Guyo alibainisha kuwa Tubi Mohamed Tubi, ambaye awali aliidhinishwa na wazee kutoka jamii mbalimbali, ndiye anayefaa kumalizia muda uliosalia wa muhula wa marehemu baba yake.
Gavana Guyo pia aliandamana na mtangulizi wake Godana Doyo, na waliokuwa wabunge wa Isiolo Kusini Abdi Koropu Tepo na Abdullahi Banticha ambaye pia ni Spika wa Bunge la Kaunti ya Isiolo.
Kwa upande mwingine, mgombea wa Jubilee, Bina Tubi, hajapata uungwaji mkono wa wazi kutoka kwa viongozi wa kisiasa wa eneo hilo, lakini anaendelea kutafuta kura za wakazi wa Isiolo Kusini ili kumshinda kaka yake katika uchaguzi wa Alhamisi.