Maafisa wa mamlaka ya kitaifa ya kampeni dhidi ya matumizi ya pombe na mihadarati (NACADA), wamenasa lita 8,000 za kemikali haramu ya Ethanol mjini Webuye,mapema Ijumaa katika juhudi za kukabiliana matumizi ya vileo haramu.
Polisi wakishirikiana na maafisa wa KRA na maafisa wa NACADA, walisimamisha lori lililokuwa likisafirisha kemikali hiyo iliyofichwa chini ya makatoni ya maziwa.
Kulikuwa na makonteina 35 kila moja ikiwa na lita 250 za ethanol inayoshukiwa ilikuwa itumike kutengeneza pombe haramu.
Afisa mkuu mtendaji wa NACADA Antony Omerikwa, aliyeongoza oparesheni hiyo amesema kemikali hiyo ililenga kuhatarisha maisha ya watu .
Sampuli za kemikali hiyo zimepelekwa katika maabara ya serikali kwa uchunguzi zaidi.