Rais William Ruto ametuma ujumbe wa heri njema kwa jamii ya Waislamu hapa nchini wanaposherehekea Siku Kuu ya Eid-ul-Adha leo Ijumaa.
“Mnaposherehekea Siku Kuu ya Eid al-Adha, Mwenyezi Mungu awape amani na furaha tele,” alisema Rais Ruto kupitia ukurasa wa X.
Maadhimisho hayo yanadhihirisha kujitolea kwa mtume Ibrahim kutoa mwanawe wa kiume, kama kafara kwa mungu kabla ya mungu kutoa kondoo kuchinjwa kama kafara.
Serikali siku ya Jumatano ilitangaza rasmi Ijumaa itakuwa likizo ya umma, kuadhimisha Eid al-Adha
Kupitia arifa maalum kwenye gazeti rasmi la serikali, waziri wa Usalama wa Taifa Kipchumba Murkomen alitangaza likizo hiyo ili kutoa fursa kwa jamii ya waisilamu kuadhimisha sherehe hiyo muhimu ya Eid-ul-Adha hii leo.