AU, WFP kushirikiana kuangazia chanzo cha migogoro

Martin Mwanje
2 Min Read

Tume ya Umoja wa Afrika kupitia kwa Sekretariati ya Hazina ya Amani, imetia saini Makubaliano na Mpango wa Chakula Duniani, WFP wa kuongeza usaidizi wa kiufundi na kifedha uliopo sasa hadi kwa shughuli mbalimbali za amani na usalama katika nyanja husika za utendaji kazi chini ya Hazina ya Amani ya AU.

Chini ya makubaliano hayo, Sekretariati ya Hazina ya Amani na WFP kwa pamoja zilitambua nyanja za kushirikiana kimkakati ili kuongeza maonyo ya mapema, uzuiaji wa migogoro na upatanishi.

Katika mpangilio wa hivi karibuni, Sekretariati ya Hazina ya Amani na WFP zitaongeza jitihada za utetezi juu ya uhusiano kati ya migogoro na usalama wa chakula kama njia ya utoaji wito wa kuchukuliwa kwa hatua ili kuangazia chanzo kikuu cha migogoro; kuimarisha usaidizi wa taasisi ya Sekretariati ya Hazina ya Amani na kuongeza ushirikiano juu ya diplomasia ya uzuiaji na upatanishi.

Akiakisi uhusiano kati ya migogoro na maendeleo, Mkurugenzi wa Sekretariati ya Hazina ya Amani, Dagmawit Moges alisisitiza umuhimu wa ushirikiano wa pande mbili na washirika wa maendeleo kuhakikisha mianya iliyopo kwenye hatua za uzuiaji inashughulikiwa ili kuepusha majanga na ukosefu wa uthabiti, sambamba na uchukuaji wa hatua za haraka kila wakati panapotokea majanga barani Afrika.

“Makubaliano yetu leo yanathibitisha uhusiano uliopo kati ya amani na maendeleo. Bila amani na usalama, hatuwezi kuwa na maendeleo endelevu na hatutapiga hatua kubwa katika uangamizaji wa umaskini,” alisema Moges.

Mkurugenzi huyo alisisitiza haja ya kumaliza vita barani Afrika ili kuwe na amani ya kudumu na maendeleo jumuishi kwa lengo la kuimarisha maendeleo ya bara hilo na hivyo kufikia Ajenda ya Mwaka 2063.

Sekretariati ya Hazina ya Amani ipo katika hatua za mwisho za utekelezaji wake. Fedha hizo zimepangwa kutumiwa kwa mara ya kwanza mwaka 2023 kwa mipango mbalimbali ikiwa ni pamoja na mzozo uliopo nchini Sudan, Misheni ya Mpito ya AU nchini Somalia (ATMIS), na Kikosi cha Kikanda cha Jumuiya ya Afrika Mashariki.

 

TAGGED:
Share This Article
Leave a Comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *