Mwanasiasa na Mbunge wa awali wa Kawempe Kusini, nchini Uganda Mubarak Munyagwa, amekanusha madai kwamba ana chuki binafsi dhidi ya mwanamuziki King Saha.
Kiongozi huyo anasema wao sio wapinzani, hivyo hawana sababu ya kuwa na uhasama.
Akizungumza katika mahojiano, Munyagwa alieleza kuwa hajawahi kujiona akiwa katika ushindani na kiongozi huyo wa KingsLove Empire, ambaye alimwelezea kuwa mmoja wa wanamuziki wenye vipaji vya kipekee na wanaopendwa zaidi nchini Uganda.
Munyagwa alifafanua kwamba mzozo kati yao uliotokea hadharani ulitokana na kauli ambazo King Saha alitoa wakati alikuwa akiwania urais.
“Tuliporushiana maneno, nilikuwa namjibu tu kwa sababu nilipogombea urais, alijaribu kunionyesha kama mtu dhaifu. Nilichomwambia ni kwamba abaki kwenye eneo lake” alielezea mwanasiasa huyo.
Munyagwa aliendelea kufichua kuwa mtazamo wake kuhusu mwanamuziki huyo ulibadilika baadaye baada ya kushuhudia matendo kadhaa yaliyoonyesha tabia yake nje ya muziki.
Alisema aliguswa alipomuona King Saha akiwa na binti yake, akitoa chakula msikitini na pia alipomsikia akieleza kwa uwazi masikitiko yake wakati wa mabishano yake ya hadharani na Mheshimiwa Kasolo.
Munyagwa alisisitiza kuwa hana tatizo lolote binafsi na King Saha na akahimiza wapenzi wa muziki kujitokeza kwa wingi kuhudhuria tamasha lijalo la mwanamuziki huyo.
Pia alikiri kuwa yeye ni shabiki wa muziki wa King Saha na anazifahamu nyimbo zake nyingi, akiongeza kuwa mabishano yao ya wakati huo ndiyo yaliyomfanya ashindwe kusema hadharani mambo mazuri kumhusu.